Header Ads

CHF Mkombozi wa kweli kwa afya ya Jamii

Na Jacquiline Mrisho - MAELEZO

Ni jambo lisilopingika kokote duniani kuwa afya   bora ndio chanzo cha maendeleo ya mtu binafsi na taifa kwa ujumla.

Afya ikiwa bora binadamu anakuwa na uwezo wa kuwaza na kufanya mambo mbalimbali yenye tija kwake na kwa taifa lake.

Kwa kuonyesha kujali afya zetu, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kupitia Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) ilianzisha Mfuko wa Afya ya Jamii  ujulikanao kama CHF ambao ulianza kwa majaribio wilayani Igunga, Mkoa wa Tabora mwaka 1996 na kuanza rasmi 2001 baada ya bunge kupitisha muswada huo.

Chimbuko hasa la kuanzisha Mfuko wa Afya ya Jamii ni kupungua kwa rasilimali na vyanzo vya mapato vya kuhudumia sekta ya afya hivyo kusababisha kudorora kwa huduma hiyo ambapo inasababisha wananchi kutopata matibabu yanayotakiwa na wengine kuacha kabisa kwenda kupata huduma katika vituo vya afya kwa kuwa gharama za matibabu ni kubwa.

Mfuko wa Afya ya Jamii yaani CHF ni utaratibu wa hiari unaomuwezesha mtu binafsi,vikundi au kaya kupata huduma za matibabu kwa mwaka mzima kwa kuchangia kiasi cha shilingi 5000 hadi 20000 kwa kadri ya  uwezo wa mtu au jamii yenyewe kulingana na Halmashauri husika itakavyoamua.
 
Kiasi hiki cha kuchangia kwa mwaka kinaweza kupatikana hata kwa mtu mwenye kipato cha chini kwakua kiwango hiki ni sawa na bei ya kuku mmoja, uchangiaji huu ndiyo uliyomfanya aliyekuwa mkuu wa Wilaya ya Iramba, Mhe. Yahaya Nawanda kuja na kauli mbiu isemayo “Kuku mmoja, matibabu mwaka mzima”. Uhamasishaji huu ulisaidia sana watu wengi kujiunga na CHF katika wilaya hiyo.
 
Na kama iliwezekana katika Halmashauri ya Iramba kwa kuku mmoja kugharamia matibabu ya kaya kwa mwaka mzima, tunaamini kuwa kauli mbiu hiyo inaweza kufanya kazi pia katika Halmashauri nyingine iwapo kila kiongozi aliyekabidhiwa dhamana ya kusimamia maisha ya watu atadhamiria kuwapa wananchi huduma bora za matibabu kwa utaratibu wa kuchangia kabla ya kuugua.

No comments:

Powered by Blogger.