UZINDUZI WA STIKA MAALUM YENYE UJUMBE WA KUTOKOMEZA MAUAJI YA ALBINO
Na Nyakongo Manyama-MAELEZO
TAASISI ya  watu wenye ulemavu wa
 ngozi mkoa wa Dar es salaam inatarajia kufanya uzinduzi wa  ‘stika’ 
maalum yenye ujumbe wa kutokomeza mauaji ya watu wenye albinism 
utakaofanyika januari 26 mwaka huu.Akizungumza na waandishi wa 
habari leo jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa taasisi hiyo Bw. Michael 
Lugendo amesema kuwa uzinduzi huo utafanyika katika kituo cha polisi 
kati jijini Dar es Salaam kuanzia saa tano asubuhi.
Bw. Michael Lugendo amesema kuwa 
stika hiyo ina lengo la kuhamasisha jamii kuungana na Rais Mhe.Dkt. John
 Pombe Magufuli na Jeshi la Polisi Kanda maalum ya Dar es salaam ili 
kuyafanya mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi yatokomezwe na yabaki 
kuwa historia.
Kwa upande mwingine Bw. Lugendo 
ameongeza kuwa kulingana na kasi ya mabadiliko tabia nchi, jamii 
isipochukua hatua za makusudi kuna uwezekano wa watu wenye ulemavu wa 
ngozi kuangamizwa na saratani ya ngozi.
Alisema watu wenye ulemavu wa 
ngozi wanaishi katika mazingira ya umaskini kiasi kwamba waliowengi 
hawana uwezo wa kupata fedha ya kununua mafuta ya kuzuia mionzi ya jua  
ambayo husababisha saratani ya ngozi.“Sisi watu wenye ulemavu wa ngozi
 ni wahanga wakubwa sana na jamii isipochukua hatua za makusudi upo 
uwezekano wa kuangamizwa na saratani ya ngozi ukizingatia kwamba 
tunaishi katika mazingira ya umaskini na walio wengi hatuna uwezo wa 
kupata fedha ya kununua mafuta” alisema Bw. Lugendo.
Aidha Bw. Lugendo amesema kuwa  
taasisi hiyo imemteua Bw. Mbwana Ally Samata kuwa balozi wa kudumu wa 
kusemea watu wenye ulemavu wa ngozi.
Alibainisha kuwa majukumu ya 
Nahodha huyo wa Timu ya Taifa ya Tanzania kwa ujumla ni kuhamasisha 
dunia kwa njia ya soka kuhakikisha  kwamba hakuna mlemavu wa ngozi 
anayefariki kwa kifo cha saratani ya ngozi au mauaji ya kukatwa viungo 
yanayotokana na Imani za kishirikina.
Bw. Lugendo aliwataka wadau 
mbalimbali, kampuni, balozi mbalimbali, Mashirika yasiyokuwa ya Serikali
 kujitokeza ili kuwezesha kutimiza lengo hilo kwa kutoa taarifa za 
uhalifu dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi kupitia vyombo vya habari 
pamoja na jeshi la polisi.
No comments:
Post a Comment