Header Ads

HOTUBA YA WAZIRI MKUU PINDA YA KUAHIRISHA MKUTANO WA 18 WA BUNGE

HOTUBA YA MHESHIMIWA MIZENGO P.  PINDA (MB), WAZIRI MKUU WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, WAKATI WA KUHITIMISHA SHUGHULI ZA MKUTANO
WA 18 WA BUNGE LA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
TAREHE 7 FEBRUARI, 2015
I:          UTANGULIZI 
(a)      Masuala ya jumla
Mheshimiwa Spika,
1.            Tumekuwepo hapa kwa takriban siku 12 katika shughuli za Mkutano wa 18 wa Bunge lako Tukufu. Ni jambo la kumshukuru Mwenyezi Mungu mwenye wingi wa Rehema kwa kutufikisha salama siku ya leo.
2.            Lakini tumekutana hapa tukiwa tumeshuhudia mabadiliko katika Baraza la Mawaziri na Wenyeviti wa baadhi ya Kamati za Kudumu za Bunge. Niruhusu nitumie nafasi hii ya awali kuwapongeza Mawaziri na Naibu Mawaziri wote ambao wameteuliwa kushika nyadhifa mbalimbali katika mabadiliko hayo. Aidha, napenda niwapongeze Wenyeviti watatu pamoja na Makamu mmoja kwa kuchaguliwa kuongoza Kamati za Kudumu za Bunge ikiwemo Kamati ya Bajeti, Kamati ya Nishati na Madini na Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala. Tunawatakia afya njema Mawaziri, Naibu Mawaziri na Wenyeviti wote katika kutekeleza majukumu yao mapya.
Mheshimiwa Spika,
3.            Tangu tulipomaliza Mkutano wa 16 na 17 wa Bunge lako Tukufu, kumetokea majanga katika sehemu mbalimbali Nchini ikiwemo mafuriko na mapigano ya Wakulima na Wafugaji kule Morogoro, pamoja na ajali za barabarani. Naomba nitumie nafasi hii kuwapa pole wote walioathirika na majanga, maafa na ajali za barabarani.  Kwa wale waliopoteza maisha tunawaombea kwa Mwenyezi Mungu azilaze roho za marehemu mahala pema peponi Amina.
b)      Maswali
Mheshimiwa Spika,
4.            Katika Mkutano huu, Waheshimiwa Wabunge wamepata fursa ya kuuliza maswali ya kawaida na yale ya papo papo kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu. Jumla ya maswali 122 ya msingi na 313 ya nyongeza yaliulizwa na Waheshimiwa Wabunge na kujibiwa na Serikali.  Aidha, Maswali 15 ya msingi na 13 ya nyongeza yaliulizwa na kujibiwa kwa utaratibu wa maswali ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu.
(c)     Miswada na Taarifa Mbalimbali
Mheshimiwa Spika,
5.             Tunahitimisha Mkutano huu tukiwa tumekamilisha kazi kubwa ya kusoma na kujadili taarifa mbalimbli za Kamati za Bunge za Kisekta na zisizo za Kisekta. Kamati za Kisekta ambazo Taarifa zake zimewasilishwa na kujadiliwa na Waheshimiwa Wabunge ni zifuatazo:
i)             Kamati ya Miundombinu;
ii)            Kamati ya Nishati na Madini;
iii)           Kamati ya Ardhi, Maliasili na Mazingira;
iv)           Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji;
v)            Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala;
vi)           Kamati ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa;
vii)         Kamati ya Masuala ya UKIMWI;
viii)        Kamati ya Ulinzi na Usalama;
ix)           Kamati ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa;
x)            Kamati ya Huduma na Jamii; na
xi)           Kamati ya Maendeleo ya Jamii.
6.            Aidha, Bunge Lako Tukufu lilipokea na kujadili Taarifa za Kamati zisizo za Kisekta zinazosimamia Fedha za Umma zifuatazo:
i)             Kamati ya Hesabu za Serikali;
ii)            Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa; na
iii)           Kamati za Bajeti.
Mheshimiwa Spika,
7.            Vilevile, tumepokea na kujadili taarifa ya Kamati Teule ya Bunge iliyoundwa kuchunguza sababu za migogoro baina ya Wakulima, Wafugaji Wawekezaji na Watumiaji wengine na Ardhi Nchini.

No comments:

Powered by Blogger.