Header Ads

ZANZIBAR NA OMAN KUSHIRIKIANA KIELIMU



 Na Maua Ally  .
                                                            
Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali imetaja majina ya wanafunzi  saba wa   Zanzibar   waliochaguliwa kujiunga na masomo ya shahada ya kwanza katika fani mbali mbali kupitia mpango  wa masomo unaodhaminiwa na Serikali ya Oman (OAF).    
  
Akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake Mazizini baada ya kumaliza ziara ya siku nne nchini Oman, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Ali Juma Shamhuna amesema wanafunzi hao wamepatikana baada ya kuwafanyia mchujo  zaidi ya vijana 300 walioomba nafasi hizo.

Amesema kamati  kutoka pande mbili,  Zanzibar na Oman, ilikaa pamoja kupitia majina ya wanafunzi wote walioomba  na kuchangua vijana saba  waliofanya vizuri zaidi katika mitihani yao na hivi sasa wanatafutiwa vyuo vya kusoma katika nchi za Ulaya na Marekani .

Waziri wa Elimu  na Mafunzo ya  Amali amesema vijana waliotakiwa  kuomba nafasi hizo ni waliomaliza kidato cha sita mwaka 2013 na kupata daraja la kwanza na la pili. Amewataja vijana hao kuwa ni Adam Kassim Ali  atakaesoma Uhandisi wa  uchimbaji  mafuta, Al- Kassim Mohd Nassor El Mazrui atakaechuka fani ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano na Khadija Hilal  Al Habsy atakaesoma Sayansi na Hesabu.

Wengine ni Mize Burhan Omar na Juwairia Mohd Ali ambao  watasoma Medicine, Ahmed Makame Mwadini na Salma Mohd Ali watakaochukua masomo ya  ufamasia. Waziri Shamhuna amewapongeza wanafunzi wote waliochaguliwa na kuongeza kuwa kuteuliwa kwao kunatokana na uwezo uliotokana na matokeo mazuri ya mitihani yao.

Ametoa wito kwa wanafunzi wengine wa kidato cha sita ambao watafanya mitihani yao mwaka huu wajitahidi kusoma kwa juhudi na kufanya vizuri ili waweze na wao kuomba nafasi hizo za masomo na hatimae kuchaguliwa.
Waziri wa Elimu amesema Serikali ya Oman itaendelea kugharamia nafasi za masomo kwa wahadhiri wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar SUZA na wafanyakazi wengine ambapo watakaporejea watafanya kazi SUZA.

“Nafasi hizo za masomo zitakuwa katika vyuo vikuu mashuhuri Duniani ambavyo pia wanafunzi wa Oman wanasoma,”alieleza Waziri Shamhuna.
Ameongeza kuwa tayari wazanzibari watano wameshajiunga na vyuo vikuu kwa masomo ya shahada ya uzamili na uzamivu na wengine sita wanakamilisha taratibu ili na wao waweze kujiunga mwaka huu.

Amesema kufuatia ziara hiyo, Serikali ya Oman imekubali kuongeza nafasi zaidi kwa wanafunzi kutoka Zanzibar kusoma katika Vyuo Vikuu vya Oman na kwa mwaka huu mwanafunzi Omar Juma Omar ameshajiunga na Chuo Kikuu nchini Oman.


Aidha amesema wamekubaliana kuongeza ushirikiano katika utoaji wa mafunzo kwa walimu wa masomo ya sayansi, Hesabati na Kiingereza kwa Skuli za Sekondari na wahudumu wa maabara.  

No comments:

Powered by Blogger.