MAZUNGUMZO KUHUSU IRAN YAINGIA DURU MUHIMU

Mazungumzo
kati ya Iran na nchi zenye nguvu zaidi duniani yanaingia siku ya tatu
huku wanadiplomasia wanaotafuta ufumbuzi wa mzozo kuhusu mpango wa
kinyuklia wa Iran wakionya kuwa vikwazo vikubwa bado vipo.
Waziri wa
mambo ya nje wa Marekani John Kerry aliyesitisha ziara yake Mashariki ya
kati kuhudhuria mazungumzo hayo kuhusu Iran yanayofanyika mjini Geneva
Uswizi, ameonya kuwa bado hakuna maafikiano kwani kuna masuala muhimu
sana mezani ambayo bado hayajatatuliwa.
Kerry
amejiunga na mawaziri wenzake wa mambo ya nje kutoka Ujerumani,Ufaransa
na Uingereza, na matumaini yanaongezeka hasa baada ya taarifa kuwa
waziri wa mambo ya nje wa Urusi Sergei Lavrov anatarajiwa kuhudhuria
leo.
Kuwasili
kwa Lavrov kutawaleta pamoja mawaziri wa mambo ya nje wa nchi zote
wanachama wa kudumu wa baraza la usalama la Umoja wa Mataifa ambao kwa
muongo mmoja wamekuwa wakiujadili mpango wa utatanishi wa kinyuklia wa
Iran.
Bado hakujaafikiwa makubaliano
Hapo
jana, Kerry,mwenzake wa Iran Javad Zarif na mkuu wa sera za kigeni wa
umoja wa Ulaya Bi Catherine Ashton anayeziwakilisha nchi sita zenye
nguvu zaidi duniani katika mazungumzo hayo walikutana hadi usiku.
Mkutano
huo uliishia kwa Kerry kusema kuwa bado kuna kazi kubwa inayowakabili
kabla ya kuafikiana.Mkutano huo unatarajiwa kuendelea leo asubuhi.
Ikiwa
makubaliano yatafikiwa ,basi hatua hiyo itakuwa ya kuuondoa mkwamo ambao
umekuweko kwa muongo mzima kati ya Iran na nchi hizo sita
zinazojumuisha Ufaransa,Uingereza,Urusi,China,Marekani na Ujerumani.
Makubaliano
yanayotarajiwa, yanayozingatiwa kuwa hatua ya kwanza ya kulifikia
suluhisho, yatakuwa na maana ya Iran kuzisimamisha shughuli zake za
kinyukilia kwa muda wa miezi sita ,ili vikwazo vilivyoubana uchumi wa
nchi hiyo vilegezwe.
Ripoti
zinaarifu kuwa makubaliano yanayopendekezwa huenda yakawa na maana ya
Iran kuacha kuyarutubisha madini ya urania kwa asilimia 20.
Je Iran itakubali kusitisha mpango wa kinyuklia?
Kiwango
hicho ni hatua chache tu kufikia uwezo wa kuunda silaha za nyuklia.Kwa
mujibu wa mapendekezo yanayotarajiwa Iran pia itapunguza milundiko ya
madini ya urania na kukubali kuacha kukifanyisha kazi kinu chake cha
plutonium cha Arak.
Lakini
mapendekezo hayo yamepingwa vikali na Israel.Waziri mkuu wake Benjamin
Netanyahu ameitaka jumuiya ya kimataifa kutozingatia kulegeza vikwazo
dhidi ya Iran kwani anahoji ,kufanya hivyo ni kuinufaisha Iran na
jumuiya ya kimataifa itakuwa imepoteza.
Marekani
imezipinga shutuma hizo za Israel kupitia msemaji wa ikulu Josh Earnest
aliyesema bado hakuna maafikiano yoyote na ameeleza kuwa kwa sasa kutoa
shutuma ni mapema mno.Taarifa kutoka ikulu hiyo imesema Rais Barrack
Obama alimpigia simu Netanyahu kutokana na matamshi yake.
Iran
imekuwa ikikanusha mara kwa mara madai kuwa mpango wake huo wa kinyuklia
ni kwa minajili ya kuunda silaha. Wakati wote imekuwa inasisittiza kuwa
mpango wake ni wa amani na wa matumzi ya nishati ya nchi yake.
Tangu
kuingia madarakani kwa Rais Hassan Rouhani mwaka huu,hatua muhimu
zimepigwa katika kutafuta ufumbuzi wa mzozo huo wa muda mrefu.
Iran
inakusudia kuuboresha uchumi wake hasa kwa mapato yatokanayo na uuzaji
wa mafuta yake ambao kwa sasa umekwamishwa na vikwazo vilivyowekwa hasa
na nchi za magharibi.
Nazo nchi
za magharibi zinatumai kuchukua fursa hiyo ya nadra kuboresha uhusiano
wa kidiplomasia na Iran ili pia kufungua milango ya majadiliano ya
masuala mengine muhimu kama mzozo wa nchi jirani Syria ambako Iran
imekuwa ikimuunga mkono Rais Bashar al Assad dhidi ya waasi wanaotaka
kumng'oa madarakani.
Mwandishi:Caro Robi/afp/Reuters
No comments:
Post a Comment