Header Ads

Simba Sumu Ya Mtibwa Sugar

WEKUNDU wa Msimbazi, Simba ambao ni mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Bara, jana walifanikiwa kujiongezea pointi tatu katika kampeni yao ya kutetea ubingwa baada ya kuifunga Mtibwa Sugar bao 1-0 kwenye Uwanja wa Jamhuri, mjini hapa.
Mechi hiyo iliyokuwa imegubikwa na kila aina ya ushindani kabla na ndani ya dakika 90, bao pekee ambalo limeiwezesha Simba kufikisha pointi 15, lilifungwa kwa mkwaju wa penalti katika dakika ya 60.
Penalti hiyo ambayo ilikwamishwa wavuni na Rashid Gumbo na kumwacha kipa Shaaban Kado akiwa hana la kufanya, ni baada ya Emmanuel Okwi kuchezewa vibaya na Obadia Mwangusa, hivyo mwamuzi Alex Mahagi kutoka Mwanza kuamuru penalti.
Bao hilo liliongeza kasi ya mchezo kwani wakati Simba wakipambana kutaka kuongeza bao, Mtibwa Sugar iliyo chini ya Kocha Mkenya Tom Olaba ilicheza soka ya hali ya juu ikitaka kusawazisha bao hilo kama si kuibuka na ushindi, lakini Simba walikuwa makini kuokoa hatari.
Kocha Olaba alifanya mabadiliko kadhaa akiwatoa Masoud Ally na Thomas Mourice na kuwaingiza Omari Matuta na Zuberi Katwila huku Simba ikiwatoa Jery Santo na Amri Kiemba wakiwapisha Juma Nyosso na Mussa Hassan Mgosi.
Mabadiliko hayo ya pande zote hayakuweza kubadili sura ya mchezo kwani licha ya kuwepo kwa mashambulizi makali kila upande, hadi filimbi ya mwisho, Simba ndio walikuwa wababe kwa bao hilo moja.
Kwa ushindi huo, Simba imefikisha pointi 15 na kufanikiwa kupunguza pengo la pointi kati yake na mtani wake Yanga yenye pointi 16 huku kila moja ikiwa imecheza mechi sita tangu kuanza kwa ligi hiyo Agosti 21.
Katika mechi sita, Yanga imeshinda tano na kutoka sare moja huku Simba ikishinda tano na kufungwa moja huku Mtibwa Sugar mabingwa wa ligi hiyo mwaka 1999 na 2000, ikibaki na pointi tisa.
Akizungumza baada ya mechi hiyo, Kocha wa Simba Mzambia Patrick Phiri aliwapongeza vijana wake kwa kucheza kwa juhudi hadi kupata ushindi kwani mechi ilikuwa ngumu kutokana na ubora wa wapinzani wao Mtibwa Sugar.
Naye Olaba wa Mtibwa Sugar, amesema licha ya kufungwa, wachezaji wake wanastahili pongezi kwa kiwango kizuri na kusema anaamini timu yake itafanya vizuri katika mechi zijazo za ligi hiyo.
Katika hatua nyingine, mashabiki wa Simba waliokuwa wakisafiri kutoka Dar es Salaam kwenda Morogoro kwa ajili ya mechi hiyo walipata ajali wakiwa eneo la Mkuza, Kibaha, baada ya basi dogo walilokuwa wamepanda kupinduka mara tatu wakati dereva akijaribu kukwepa gari jingine.
Hadi tunakwenda mitamboni, habari zilisema kuwa majeruhi wengi waliokuwa wamepelekwa kwenye Hospitali ya Tumbi, Kibaha kwa matibabu walikuwa wameruhusiwa isipokuwa watu watano.
Kutoka Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, jijini Arusha, timu ya Toto Africa jana ilivuna pointi tatu baada ya kuwatandika vibonde wa ligi hiyo AFC kwa bao 1-0, likifungwa dakika ya 68 na Jacob Massawe kutokana na pasi ya Emmanuel Switta.
Naye Mwandishi Wetu, Safari Chuwa anaripoti kutoka Uwanja wa Mkwakwani, mjini Tanga kuwa timu ya Azam FC ya Dar es Salaam ingawa inautumia uwanja huo kama wa nyumbani, ilitoka sare ya bila kufungana na maafande wa JKT Ruvu ya Pwani.
Licha ya timu hizo kushambuliana kwa nguvu, lakini zilijikuta zikimaliza dakika 90 bila kupata bao, hivyo kugawana pointi.

No comments:

Powered by Blogger.