Header Ads

Dola za Marekani Milioni 132 kutumika mradi mkubwa wa umeme wa upepo wa Megawati 50 Singida. Kutoa ajira 2,200

 
 
Mwenyekiti wa Kamati  ya Kudumu ya Bunge ya  Nishati na Madini, Richard Ndassa akitoa maagizo kwa Wakandarasi, Wataalamu kutoka  Shirika la Umeme Nchini (Tanesco), Wizara ya Nishati na Madini na  viongozi mbalimbali kwenye majumuisho  ya ziara ya kamati hiyo, baada ya kufanya ukaguzi wa miradi ya umeme mkoani Singida pamoja na kuzungumza na wananchi.
Mwenyekiti wa Kamati  ya Kudumu ya Bunge ya  Nishati na Madini, Richard Ndassa (katikati) akisisitiza  jambo  katika eneo la mradi wa kuzalisha umeme kwa njia ya  upepo lililopo Kisesile wilayani Singida Mjini  mara  kamati hiyo  ilipotembelea mradi huo ili kujionea maendeleo yake pamoja na kuzungumza na watendaji wa eneo hilo.
Na Greyson Mwase, Singida.

Mkuu wa Kitengo cha Miundombinu  na  Nishati  kutoka Shirika la Maendeleo la  Taifa (NDC)  Pascal Malesa  amesema kuwa serikali inatarajia kutumia   Dola za Marekani  Milioni 132 kwa ajili ya kukamilisha mradi wa kuzalisha umeme wa upepo wenye uwezo  wa Megawati 50 ifikapo  mapema mwaka 2016.

Malesa aliyasema hayo mbele ya Kamati ya  Kudumu ya Bunge  ya Nishati na Madini  iliyofanya ziara ya kutembelea mradi wa kuzalisha  umeme kwa njia ya upepo unaojengwa  katika eneo la  Kisesile  nje kidogo ya  Singida  Mjini. Kamati ya  Bunge ya Nishati na Madini  ipo mkoani  Singida kwa ajili ya kukagua miradi ya umeme ili kujionea maendeleo yake pamoja na kuzungumza na wananchi.

Alisema mradi huo  unatekelezwa kwa ubia kati ya  Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) lenye asilimia 60, Shirika la Umeme Nchini (Tanesco) lenye  asilimia 20 na kampuni ya  Power Pool  East  Africa Limited yenye asilimia 20 chini ya kampuni ya ubia iitwayo  Geo  Wind Power  Tanzania  Limited  (Geo Wind)  iliyoundwa mwaka 2011.

Malesa alieleza kuwa gharama hizo zinahusisha utekelezaji wa mradi huo  awamu ya kwanza kwa ajili ya kuzalisha megawati 50 ambayo itahusisha ujenzi  wa msongo wa umeme  wa kilovolti 220 umbali wa kilomita 12 na kuunganisha kwenye  gridi ya  taifa.

Alisema  fedha hizo ni  mkopo kutoka  Benki ya  Exim  ya  China na  kuongeza  kuwa kwa  sasa Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) linafuatilia mkopo  huu chini  ya  udhamini wa Serikali  kupitia  Wizara ya  Fedha  baada ya kukamilisha  vigezo vyote  vya mradi vilivyotolewa na benki hiyo kwa ajili ya kupata mkopo  wa masharti nafuu na kuviwasilisha benki ya Exim ya  Serikali ya watu wa  China.

No comments:

Powered by Blogger.