Header Ads

Tamko la Mhe. Nyalandu kuhusu shutuma za Mbunge Mhe. Nassari



“Nimesikitishwa sana na kauli ya Mhe. Joshua Nassari ambayo ameongea kwa kudhalilisha  utendaji wangu  serikalini.  

Naomba  Mh. Nassari  afahamu kuwa  kunikashifu pasipo  kueleza masuala  ya kisera  au ya kiutendaji ni  kupungukiwa na busara  ya kawaida kwa kiongozi aliyepaswa kuwawakilisha wapiga kura wake kwa hoja.

Itakumbukwa kuwa hivi karibuni Mhe. Nassari aliniita Jimboni kwake  Arumeru Mashariki akiniomba nitatue  tatizo  lililohusu wananchi  wa  jimboni kwake waliokuwa wanahitaji matibabu katika  hospitali  ambayo ilikuwa sharti  upitie ndani  ya hifadhi  ili ufike kutibiwa.

 Nilikwenda kuwaona wagonjwa na kuitembelea hospitali hiyo na kulitatua tatizo hilo  siku hiyo hiyo.  Kwangu  kama Waziri, halikuwa suala  la  kufanyia  siasa  afya za Watanzania, pamoja na yeye kuwa Mbunge wa upinzani. 

Nilimheshimu na kukubali wito wake kwa niaba ya wananchi.  Nimewatembelea na kuwatia  moyo maaskari wetu  nchi nzima  na kuwapelekea  vitendea kazi. Nimefurahi pamoja nao  na kulia pamoja nao. Nimeenda kuwafariji familia za wapiganaji  wetu waliopoteza maisha kwa kuuawa wakilinda raslimali za Taifa, watu ambao  Mhe. Nassari anawabeza. 


Tumepambana na ujangili na tunaendelea kuushinda. Tumeleta magari, silaha,  ndege, helicopters, na raslimali nyingi ili kulinda raslimali za Taifa.  Busara haisomewi ila ni kumshukuru Mungu  akusaidie kujua  matumizi ya ulimi. Nimesikitishwa sana na kauli  za uongo na kuzusha za Mhe. Nassari. Imeandikwa, usimsingizie jirani yako  uongo.”

Mh. Lazaro Nyalandu.

No comments:

Powered by Blogger.